MFANYABIASHARA maarufu na kada wa Chama Cha
Mapinduzi (CCM), Mustafa Jaffer Sabodo amekichangia tena Chama cha Demokrasia
na Maendeleo (CHADEMA), sh. milioni 10, huku akitoa ahadi nyingine mpya ya
kukipatia chama hicho mradi wa kukiingizia mapato na kuchimba visima kwa majimbo
ya chama hicho kwa miaka 10.
Amesema kuwa kazi inayofanywa na chama hicho kutoa
elimu ya uraia hadi vijijini, huku kikizidi kuimarisha mtandao wake kwenye ngazi
za vitongoji na mitaa kikidhamiria kuendelea kupigania na kutetea haki za
wananchi, inapaswa kuungwa mkono na kila Mtanzania mpenda maendeleo.
Mfanyabiashara huyo ambaye amekuwa akijitokeza
waziwazi bila uoga kukichangia chama hicho cha upinzani, akisema anafurahishwa
na kazi ambayo kinafanya ya kutetea maslahi na rasilimali za Watanzania kutengeneza
fursa za maendeleo, ameongeza kuwa amefurahishwa na Operesheni Okoa Kusini,
ambayo chama hicho kilifanya karibuni mikoa ya Lindi na Mtwara.
Akizungumza jana nyumbani kwake ambako alikutana
na Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dkt. Willibrod Slaa kwa ajili ya kuzungumzia mchakato
wa utekelezaji wa ahadi alizotoa kwa chama hicho, Mzee Sabodo aliahidi kuwa baada
ya kukamilika kwa jengo la kuegesha magari linalojengwa katikati ya Jiji la Dar
es Salaam, sehemu ya mapato yatatumika kuchimba visima kwa miaka 10.
Mbali ya sehemu ya mapato kutoka katika jengo
hilo la kuegesha magari ambalo linajengwa na Taasisi ya Khoja Shia Ithnasheri
Jamaat (KSIJAMAAT), pia Mzee Sabodo alisema kuwa sehemu ya chini ya jengo hilo
ambayo itakuwa na maduka, CHADEMA itapatiwa duka moja kama mmoja wa miradi ya
kukipatia mapato.
“Mtapata sehemu ya mapato ili kuchimba visima
kwenye majimbo yenu kwa miaka kumi…pia mtapata duka pale ili mpate mradi wa mapato.
Ili kuharakisha utekelezaji wa ahadi ya visima vile vingine fanyeni survey
ninyi wenyewe na mpate mkandarasi, itakuwa sehemu ya gharama ya uchimbaji…hizi
milioni 10 mtapata hundi hapa mkafanye kazi za wananchi,” alisema Mzee Sabodo.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dkt. Slaa,
mbali ya kumshukuru na kumpongeza Mzee Sabodo kwa ujasiri wake wa kuendelea
kujitoa kusaidia harakati za kupigania haki za wananchi, mabadiliko ya
kiutawala na kimfumo nchini, aliahidi kuwa chama hicho kitaendelea kutimiza
wajibu wake kwa maslahi ya Watanzania.
“Umekuwa mtu wa msaada mkubwa kwetu, umeendelea
kuwatia moyo Watanzania wote wa kila namna kuacha uoga wa kuchangia harakati
hizi, kwani lengo letu ni kuwatumikia Watanzania katika kila fursa tunayoipata,
ambapo kwa sasa tutaendelea kuisimamia na kuiwajibisha serikali ya CCM ambayo
ni dhahiri ielekea mwisho na wananchi wameichoka.
“Nasi tunawaahidi Watanzania wote kuwa
tutaendelea kuwatumikia na hatutawaangusha, tunatambua kuwa katika
mparanganyiko huu mkubwa, kama ugumu wa maisha, hali mbaya ya uchumi, siasa
zinazoyumba, ufisadi na ubadhirifu wa mali za umma na migogoro katika makundi
mbalimbali ya kijamii kwa sababu ya uongozi mbovu, CHADEMA linabaki kuwa ndiyo
tumaini pekee kwa Watanzania,” alisema Dkt. Slaa.
Dkt. Slaa aliyeambatana na Mkurugenzi wa Fedha
na Utawala wa CHADEMA, Antony Komu, aliongeza kuwa visima vya ahadi hii mpya kutokana
na mapato ya jengo la maegesho ambayo ni tofauti na ahadi za visima vingine
alizowahi kutoa mwaka jana na mapema mwaka huu, vitachimbwa katika maeneo
mbalimbali ya Tanzania yenye kero kubwa za maji.
Mbali ya ahadi hizo mpya za jana, Mzee Sabodo na
Dkt. Slaa walizungumzia juu ya mchakato wa utekelezaji wa ahadi mbalimbali zingine
za mfanyabiashara huyo na kada wa CCM, ambazo amekuwa akitoa kwa CHADEMA mara
kadhaa tangu mwaka 2010, zikiwemo za ujenzi wa chuo, uchimbaji wa visima, ofisi
za makao makuu ya chama hicho na baiskeli 100 za walemavu.
No comments:
Post a Comment